Wanachama Simba waupitisha mfumo wa Hisa kwa kishindo
Habari Zinazoendana
HATIMAYE wanachama wa Simba leo wamepitisha kipengele cha uendeshwaji wa klabu kwa muundo wa hisa katika mkutano maalum wa mabadiliko ya Katiba uliofanyika ukumbi wa Bwalo la Maofisa wa Polisi Oysterbay, Dar es Salaam.
Kwa mujibu wa Katibu Mkuu wa klabu ya Simba SC Patrick Kahemele, zaidi ya 98% ya wanachama waliohudhuria mkutano wameunga mkono ajenda ya mabadiliko ya katiba iliyopelekwa kwenye mkutano huo wa dharura.
Katika mkutano huo ulioongozwa na Rais wa klabu, Evans Elieza Aveva na kuhudhuriwa na wanachama 642 kati ya zaidi 5,000 wa klabu hiyo – mabadiliko ya Katiba yalipita kwa kishindo.
Mabadiliko ya Kipengele cha 49.
Kabla ya kufanyiwa mabadiliko,
Ibara ya 49: Kuvunjwa na Kufutwa Simba Sports Club
(i) Uamuzi wowote wa kuvunja au kufutwa kwa Simba Sports Club unahitaji theluthi mbili za wanachama wote wa Simba Sports Club waliopatikana katika mkutano mkuu ulioitishwa maalum kwa madhumuni hayo.
(ii) Utakuwa ni mkutano maalum wa agenda hiyo pekee.
(iii) Kuwepo na sababu za kuvunja au kufutwa kwa klabu kama vile kuwa na madeni makubwa yaliyolipika, kupoteza hadhi ya kutoaminika na kukopesheka n.k
Baada ya kufanyiwa marekebisho
Ibara ya 49 Kubadilisha mfumo, kuvunja au kufutwa kwa klabu ya Simba Sports Club
(i) Uamuzi wowote wa kubadilisha mfumo, kuvunja au kufutwa kwa Simba Sports Club unahitaji theluthi mbili za wanachama wote wa Simba Sports Club waliopatikana katika mkutano mkuu ulioitishwa maalum kwa madhumuni hayo.
(ii) (KAKUNA MABADILIKO)
(iii) Kuwepo na sababu za kubadilisha mfumo, kuvunja au kufutwa kwa Simba Sports Club kama vile kuwa na madeni makubwa yaliyolipika, kupoteza hadhi ya kutoaminika na kukopesheka au kuendana na matakwa ya mfumo wa nyakati za kimichezo na au za kibiashara.
(iv) (a) Mkutano mkuu wa wanachama unaweza kuitishwa kwa mujibu wa Ibara ya 22 na kufanya mabadiliko ya mfumo wa umiliki au uendeshaji wa Simba Sports Club.
(b) Mabadiliko ya mfumo wa uendeshaji au umiliki wa Simba Sports Club hayataathiri hadhi ya wanachama wote halali wa Simba Sports Club isipokuwa hadhi hiyo itabadilika kuendana na mfumo stahiki wa mabadiliko yaliyofanyika. Uwiano wa thamani ya umiliki wa kila mwanachama katika mfumo mpya utajadiliwa na kamati ya utendaji kutokana na thamani ya klabu na uwekezaji.
(c) Mfumo mpya wa mabadiliko ya uendeshaji au umiliki wa Simba Sports Club utaathiri haki na mali zote pamoja na madeni na wajibu wowote uliokuwa chini ya Simba Sports Club kabla ya mabadiliko hayo.
(d) Mabadiliko ya mfumo wa umiliki au uendeshaji wa Simba Sports Club yatamaanisha kuacha kuacha kutumika kwa katiba hii. Mkutano mkuu chini ya mfumo mpya utapitisha katiba mpya chini ya utaratibu wa haki ya kura za mfumo huo.
Baada ya Simba kupitisha marekebisho hayo, yatapelekwa kwa Shirikisho la mpira wa miguu nchini (TFF) kwa ajili ya kupitiwa kabla ya kupelekwa Baraza la Michezo Tanzania (BMT) ili kuisajili.
Next
« Prev Post
« Prev Post
Previous
Next Post »
Next Post »
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
EmoticonEmoticon